KUSOMA KWA UFAHAMU
Kusoma Kimya
Ufahamu wa kusoma ni ule mtu anaoupata kwa njia ya kusoma makala, kifungu cha habari, kitabu au gazeti.
Maswali ya Ufahamu kutokana na Habari uliyosoma
Katika ufahamu wa kusoma, msomaji anatakiwa kuzingatia mambo yafuatayo:
- Kubaini mawazo makuu
- Kuzingatia alama za uakifishi
- Kubaini maana ya maneno na misemo mbalimbali
- Vilevile msomaji anatakiwa kumakinikia kile anachokisoma, kila kipengele anachokisoma inampasa akielewe vizuri.
Kwa kuzingatia haya yote msomaji atakuwa na uelewa mzuri juu ya habari aliyoisoma na pia anaweza kufupisha habari hiyo aliyoisoma
Kufupisha habari
Kufupisha habari ni kuandika upya habari uliyoisoma kwa maneno machache lakini bila kupotosha ujumbe wa habari ya kwanza.
Ufupisho wa habari huwa na sifa hizi:
- Huwa ni mfupi kuliko habari ya mwanzo
- Huwa na ujumbe uleule uliokuwa katika habari ya mwanzo
- Hujumuisha mawazo makuu yaliyodondolewa kutoka kwenye habari ya mwanzo
- Mawazo haya sharti yapangwe katika mtririko wenye mantiki
Hatua za kufuata katika kuandika ufupisho
Ili kuweza kufanikiwa kufupisha habari kwa ufanisi hatua zifuatzo sharti zifuatwe:
- Kuisoma au kuisilikiza habari kwa makini ili kuielewa vizuri
- Kutambua na kubaini mawazo makuu yanayojitokeza katika kila aya
- Kuyaunganisha mawazo makuu na kuandika au kuelezea ufupisho wa habari hiyo kwa maneno yako mwenyewe bila kupostosha maana ya habari ya kwanza.
- Kuhesabu idadi ya maneno ya ufupisho ili kuyapunguza ikiwa yanazidi idadi iliyotakiwa.
- Kama muda unaruhusu pitia tena habari ya mwanzo na pitia tena ufupisho ili kujiridhisha kuwa hujaacha taarifa yoyote ya muhimu.
Kufupisha Habari Uliyoisoma
Mtu mmoja na mkewe kutoka jamii ya Daliti inayobaguliwa tangu jadi nchini India wameuawa, mmoja akiwa amekatwa kichwa na mwengine kunyongwa kwa kushindwa kulipa deni la Rupee kumi na tano ambalo ni karibu senti ishirini na mbili tu.
Polisi kaskazini mwa taifa hilo wamethibitisha kisa hicho ambapo yasemekana mfanyi biashara anayetokea jamii ya hadhi ya juu,aliwaua wanandoa hao kwa kushindwa kulipa deni la biskuti walizokuwa wamewachukulia watoto wao.
Mfanyi biashara huyo amekamatwa.Ubaguzi kwa misingi ya kijamii umeenea sana nchini India, huku watu wa jamii ya Daliti waliokuwa wamebadikwa jina la ‘the untouchables’ wakiwekwa kwenye daraja la chini kabisa kwenye sera hiyo ya kibaguzi nchini India iitwayo ‘caste’ ambapo wananyimwa fursa nyingi za kimaendeleo na hivyo kubaki katika lindi la umaskini.
Hata hivyo Visa vya ukatili wa kibaguzi dhidi ya jamii ya Dalit katika jimbo la Gujarat vimeongezeka mnamo siku za hivi karibuni na vimesababisha wimbi la maandamano kutoka watu wa jamii hiyo.
Zoezi
Kwa maneno yasiyozidi 30 fupisha habari uliyoisoma hapo juu.
USIACHE KUSHARE HII POSTI NA NDUGU NA JAMAA KWA NJIA YOYOTE ILE